Wednesday, April 11, 2012

SABABU ZA KIFO CHA KANUMBA ZATAJWA

Baada ya utata kuhusiana na kifo cha nyota wa filamu Tanzania, Steven Charles Kanumba ambaye amezikwa jana katika makaburi ya kinondoni jiji Dar es salaam, hatimaye jopo la madaktari waliokuwa wakifanya uchunguzi kuhusu kifo hicho wametoa ripoti.

Jopo hilo la madaktari wapatao watano kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili wamesema kifo cha Kanumba kimetokana na tatizo la mtikisiko wa ubongo ambalo kitaalamu linafahamika kama Brain Concussion.

Taarifa zaidi zinasema kuwa tatizo hilolinaweza kumsababishia mtu kupoteza maisha mara moja au baada ya siku kadhaa ambapo taarifa zimeendelea kusema kuwa tatizo hilo liligundulika baada ya kufanyiwa uchunguzi kwa muda wa masaa mawili.

Aidha taarifa hiyo imeendelea kubainisha kuwa Kanumba alipata mtikisiko wa ubongo ambao husababisha kufeli kwa mfumo wa upumuaji ujulikanao kama Cardio-Respitory failure.
Hata hivyo baada ya uchunguzi imebainika kuwa kucha za marehemu zimebadilika na kuwa za Bluu wakati mapafu yake yalikutwa yakiwa yamevilia damu na kubadilika na kuwa kama maini.

Aidha taarifa hiyo imeendelea kueleza kuwa mtu aliyepata mtikisiko wa ubongo anaweza kutokwa na mapovu mdomoni na kukoroma kabla ya kukata roho na kuthibitisha kuwa hicho ndicho kilichotokea kwa marehemu Kanumba.

Hata hivyo mmoja wa madaktari waliofanya uchunguzi huo amesema ubongo wa marehemu Kanumba ulikuwa umevimba na kushuka karibu na uti wa mgongo na hivyo kuathiri mfumo wa upumuaji, wakati huo huo sehemu ya maini pamoja na majimaji ya machoni vimepelekwa kwa Mkemia mkuu wa serikali ili kubaini endapo kuna sumu au kitu chochote kwenye mwili wa marehemu.

No comments:

Post a Comment