Thursday, December 8, 2011

VYOMBO VYA HABARI VINACHANGIA KUUPOTEZA MUZIKI WA ASILI

John Kitime
Mwanamuziki mkongwe nchini Tanzania John Kitime amepeleka kilio chake kwa vyombo vya habari kuwa ni moja kati ya vitu vinavyochangia katika kuupoteza muziki wa asili

Akizungumza na kipindi cha Afrobeat katika kumbukumbu ya miaka 50 ya uhuru wa Tanzania Bara, na muziki wetu Tanzania Kitime alisema hayo pale alipoulizwa kwa upande wake anafikiri ni nini kinachangia kupotea kwa muziki wa asili wakati muziki wa kisasa unapanda, alisema Muziki huo haujapotea kwa sababu kuna vikundi vingi vya Muziki wa asili kama vile ngoma ambavyo vinatumbuiza katika sehemu mbalimbali lakini havisikiki kwa sababu vyombo vya habari haviutangazi na badala yake unatangazwa muziki huo wa kisasa ambao unaonekana kuwa upo juu lakini si kweli, ila ukweli ni kwamba muziki wa asili haupewi nafasi ya kutangazwa au kupigwa kwenye vyombo vya habari.

Akizungumzia kuhusu tungo za sasa hivi kuzungumzia zaidi suala la mapenzi, Kitime alisema hilo linatokana na malezi ya watoto wa sasa hivi si kama ya zamani ambapo wakati huo vijana walifundishwa kuwa Lugha ya Staha tofauti na sasa hivi vijana wanaona kawaida kutamka maneno makali hasa ya mapenzi hadharani bila Staha kutokana na namna walivyolelewa na wazazi wao na jamii inayowazunguka, akaongeza kuwa uwingi wa Studio pia unachangia tofauti na zamani ambapo studio ya kurekodia ilikuwa moja tu ya RTD ambapo ilikuwa kabla wimbo wako hujaurekodi lazima upitiwe ili kuangalia maneno uliyoyatumia na kama kuna tatizo uanaambiwa urekebishe ndipo unarekodi na kama haueleweki kabisa hauruhusiwi kurekodi lakini sasa hivi watu wako kibiashara zaidi hawazingatii mashairi.

Kuhusu suala la maendeleo ya muziki amesema sasa hivi kuna maendeleo makubwa sana kwa sababu hata jamii yenyewe imekubali kuwa muziki ni kazi kama kazi zingine ndiyo maana sasa hivi kuna wanawake wengi sana wanafanya kazi hiyo tofauti na zamani ambapo mwanamke akionekana kwenye jukwaa la muziki anaonekana ni mhuni jambo ambalo liliwakatisha tamaa wanawake wengi ingawa walikuwepo wachache waliojitoa.

No comments:

Post a Comment