Wednesday, July 31, 2013

Matapeli wa Kigeni wanaswa Kigoma

Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma linawashikilia watu wawili wenye asilia ya kiarabu na watanzania watatu kwa tuhuma za kufanya utapeli na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu katika vituo vya kuuzia mafuta (sheli) na maduka ya kubadilishia fedha.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma Bw, David Misime alisema Tukio hilo lilitokea juzi katika Sheli ya Camel Iliyopo karibu na Chuo Cha Mipango katika manispaa ya Dodoma.

Kamanda Misime alisema watu hao walifika katika sheli hiyo ambapo kulikuwa na duka na kuagiza soda kisha baadae kutoa dola ya kimarekani ya USD 50, ambapo muuzaji aliwaambia kuwa habadilishi pesa, hivyo kuamua kumdanganya kuwa wanahitaji pesa ya kitanzania kwa ajili ya kwenda kuonyesha Misri kama sehemu ya maonyesho.

“Wateja hao waliomba wapatiwe noti za 10,000/= za zamani ili wao wampatie noti mpya za 10,000/=, muuzaji huyo alichambua noti za zamani zipatazo shilingi 470,000/= na kuwapa kisha wao kumwambia wanazotaka kumbadilishia ziko kwenye gari na kujifanya kwenda katika gari na matokeo yake waliondoka kwa kasi” alieleza Kamanda David Misime

Mkuu huyo wa Polisi Mkoa wa Dodoma alisema baada ya watu hao kuondoka kwa kasi ndipo muuzaji huyo kugundua kwamba ameibiwa na kupiga simu Polisi ambao waliwasiliana na vituo vyote vya mjini na nje ya mji na kufanikiwa kuwakamata matapeli hao katika kituo/barrie ya Chanene liyopo wilayani Chamwino pori la Mtungutu.

Kamanda Misime aliwataja watuhumiwa hao waliokuwa wakitumia gari aina RAV 4 T. 872 CGE la rangi ya damu yam zee kuwa ni mwanamke Ahlam d/o Hassan, miaka hamsini mwarabu na mkazi wa Tanga, mwanaume Daoud Esam@Abdelgawad , miaka 39 , msudani dereva na mkazi wa misri ambaye alikuwa na passport ya kuiingia nchini tarehe 19/07/2013 na ana Visa ya kukaa Tanzania kwa muda wa Miezi mitatu.

Wengine ambao baada ya kuhojiwa, Kamanda alisema walikiri kufanya utapeli huo ni Matata Laurence, miaka (38) dereva na mkazi wa Gongo la Mboto, Rahma Mahamoud, miaka (26) Mkazi wa Dar es Salaam pamoja na Salehe Hamad Mnene , miaka 40 na mkazi wa Manzese Dar es salaam.

Jeshi la Polisi linatoa tahadhari kwa wanachi kuwa makini na ya watu wanaofanya vitendo vya namna hii na kuwataka kutoa taarifa mapema pindi wanapotia shaka kwa watu wa aina hiyo, ili hatua za kuwadhibiti zichukuliwe mapema.

Watukana matusi mitandaoni kuchukuliwa hatua

Wale wote watakaotukana matusi kwenye mitandao, na kupotosha umma kwa habari za uongo, TCRA inasema itawachukulia hatua.

TCRA leo imezindua kampeni maalum ya kuhamasisha matumizi mazuri ya mitandao ya kijamii na mawasiliano.

Mkurugenzi wa TCRA , Prof John Nkoma amesema lengo kampeni hiyo ni kupunguza matusi katika mitandao ya kijamii na kupotosha jami kwa habari zisizokuwa na uhakika na za kuchochea vurugu.

Pia TCRA imezindua wimbo maalum wa kampeni hiyo uitwao FUTA, DELETE, KABISA na umeimbwa naye Banana Zorro pia Mrisho Mpoto

Tuesday, July 30, 2013

Zamu ya Nape sasa! Duh

Nape Nnauye ameamua  kuvunja  ukimya  na  kutoa  utetezi  wake  kuhusu  kauli  yake chafu  iliyochapishwa  na  gazeti  la  Mtanzania  likimtuhumu  kuwatusi  wazee  waliopendekeza  uwepo  wa  serikali  tatu.....

Huu  ni  utetezi  wake:

"Nimestushwa sana na stori ya gazeti la Mtanzania inayodai kuninukuu kuwa nimesema wazee waliopendekeza serikali tatu wanasubiri kufa!
Kwakweli nimesikitishwa sana hata na jinsi maneno ndani yalivyopangiliwa kiasi kwamba inanipa tabu kuamini kama mhariri aliipitia hii stori ukiachilia mbali kama aliyetumwa kuja kuandika stori alikuwa ni "too junior".
Nawaheshimu sana wazee wangu hawa hata kama nikipishana nao kimawazo siwezi kufikia kutamka maneno makali kiasi hicho.
Nilichosema ni kuwa ukilinganisha vijana na wazee, vijana wana wajibu mkubwa wa kuamua kesho yao badala ya kudhani kuna mtu atawaamulia. Hivyo wana wajibu mkubwa kwani takwimu zinaonyesha asilimia 60% ya idadi ya watu nchini ni vijana! Sasa sijui kama kwa mwandishi na mhariri wake tafsiri ndio hiyo?!!!
Imenisikitisha  sana!
Nape Moses Nnauye
The CCM Secretary for Ideology & Publicity"

ISHU NZIMA ILIVYOANZA:

MZIMU wa serikali tatu bado unaendelea kukitesa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo jana, Katibu Mkuu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alipinga tena uwepo wa serikali tatu na kudai kuwa waliotoa maoni hayo ni wazee wanaosubiri kufa.


Akizungumza jijini Dar es Salaam katika kongamano la Umoja wa Vijana (UVCCM) la kujadili mchakato wa Katiba Mpya, katika ukumbi wa Arnatouglo, Nnauye alisema nia ya serikali tatu ni kuleta matabaka ambayo yatasababisha migogoro.

“Wazee hawa wanaosubiri kufa wanataka kutuletea matabaka, vijana ndio nguvu kazi ya taifa, kitendo cha kuwepo kwa serikali tatu ni kusababisha mgogoro, kwa nini wasingevunja Muungano enzi za ujana wao? Wamenufaika na Muungano kwa kipindi cha miaka 50, sisi vijana wanataka kutuachia mgogoro!”alisema Nnauye.

Nape alisema kuvunjwa kwa Muungano kutasababisha mgogoro mkubwa wa rasimu kutokana na muda ambao Muungano huo umedumu.

Alisema kuundwa kwa serikali tatu si sera ya CCM kama wanavyodai wapinzani, bali ni maoni ya watu waliyoyawasilisha katika ukusanywaji wa maoni ya Rasimu ya Katiba mpya.

“Sera ya CCM ni kuongoza serikali mbili na si tatu, na hii sera tutaendelea kuitetea na kuilinda mpaka mwisho wa dunia, tunachoamini katika chama chetu hatuogopi kutetea sera ambazo tumezitoa wenyewe,” alisema Nnauye.

Alisema ni vyema zikamalizwa kasoro zilipo katika mfumo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na si kuongeza madaraka yasiyo na tija.

Nape alisema kitendo cha Tume ya Jaji Joseph Warioba kusema imetumia sheria ya mwaka 1964 kuwa kigezo cha kuundwa kwa serikali tatu si sahihi, kutokana na makubaliano ya mwaka huo kwamba ni serikali mbili.

Kiongozi huyo wa CCM pia alishangazwa na kitendo cha Rasimu ya Katiba mpya kutamka wazi idadi ya mikoa pamoja na wilaya ambazo zitatumika katika uchaguzi na kwamba mwenye jukumu hilo ni Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein.

“Serikali ya Muungano chini ya mfumo wa serikali tatu itaelea katika madaraka, kwani serikali ya Tanganyika itakuwa haiwezi kuwatetea wananchi, hali itakayosababisha kuwepo kwa mgogoro mkubwa wa urasimu ambao ni adui wa maendeleo,” alisema Nnauye.

Aidha alisema kuwa kuvunjika kwa Muungano kutasababisha kuiburuza Serikali ya Zanzibar kiuchumi, kwani asilimia 95 ya uchumi wa visiwani unategemea Tanzania Bara.

Alisema kuwa sera nzuri ya kuwa kiongozi ni kuwatetea wananchi na si kuwazidishia mizigo.

Akizungumzia suala la mgombea binafsi, Nnauye alisema CCM hakiogopi mgombea binafsi, kwani hata akigombea chama hakitapata hasara yoyote.

Nape alisema sera ya CCM ni kukataa wagombea binafsi wanaouza unga na si kukataa mgombea binafsi kama ambavyo vyama vingine vya siasa vinavyodai katika vyombo vya habari.

Alisema katika Rasimu hiyo sura ya 9 inazungumzia umri wa Mbunge kuwa kuanzia miaka 25, lakini kwa CCM suala hilo si sahihi, kwani wabunge wenye miaka 21 wanawajibika vizuri kuliko wazee.

Monday, July 29, 2013

Vigogo wa Unga Tanzania, watajwa!





Mbunge Wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania ametajwa na wafungwa wa kitanzania waliofungwa jela huko nchini Hong Kong kuhusika na biashara ya madawa ya kulevya.

Taarifa hiyo iliyomhusisha Mbunge huyo na mtandao huo mkubwa wa biashara hiyo ya madawa ya kulevya nchini Tanzania, ilitolewa katika barua maalum iliyoandikwa na mmoja wa Wafungwa katika magereza ya nchini Hong Kong ambapo inasemekana kuna wafungwa wa kitanzania wanaofikia 200.

Kati ya hao wafungwa 200 waliopo magerezani na vizuizini, 130 tayari wameshahukumiwa na 70 bado wanasubiri kesi zao kutajwa. Kuanzia Mwezi wa Tano mpaka wa Sita mwaka huu wa 2013, tayari Watanzania wapatao 50 wameshakamatwa na madawa ya kulevya wakati wakijaribu kuingia katika viwanja vya ndege vya nchi za China na Hong Kong.

Mbali na Hong Kong, pia kumekuwepo na taarifa mbalimbali za raia wa Tanzania ambao wamekatwa na madawa ya kulevya nchini Afrika ya Kusini na kwingineko duniani. Mmoja kati ya waliokamatwa na madawa hayo ni mwanadada mahiri wa Kitanzania ambaye alikuwa mrembo katika video mbalimbali za Bongo Flava anayeitwa Agnes Gerald au kama anavyojulikana na wengi kwa jina la Masogange.

Waraka huo wa mfungwa huyo wa Kitanzania pia umeorodhesha idadi kubwa ya wafanyabiashara wengine nchini Tanzania ambao ni wahusika wakubwa katika biashara hii haramu ya madawa ya kulevya.

Madawa hayo ya kulevya yanasemekana yanaingizwa nchini Tanzania kwa wingi kwa njia ya meli na boti mbalimbali yakitokea katika nchi za Pakistan, Afghanistan na nchi nyingine za Mashariki ya mbali.

Ni muhimu kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuanzisha kampeni kubwa ya kuwakamata wahusika wote katika biashara hii na kuwafikisha katika vyombo vya sheria, athari za madawa hayo zimezidi kuonekana sehemu mbalimbali nchini Tanzania na dunia nzima.

Thursday, July 25, 2013

Aliyefukuzwa kanisani akiwa na vazi la nusu uchi asema kanisa limemuonea gere na wamemharibia viatu vyake vya Uingereza..!!!

Wakati mwanamke wa kivazi kilichositisha ndoa kanisani kwa dakika kadhaa akidai hakuwa na tatizo kuvaa vile, Katekista wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Peter, Yohane Maboko, amesisitiza kuwa alikiuka maadili ya Kanisa.

Mwanamke huyo ambaye ameendelea kukataa kutaja jina lake, huku njia zingine zikimtaja kwa jina la Restituta Kalemera, alidai juzi kuwa kivazi hicho cha mabega wazi hakikuwa tatizo kanisani, bali ni unyanyasaji tu wa Katekista huyo.


Akizungumza  juzi, alidai kuwa Katekista Maboko alimsukuma na kumwangusha katika ngazi ndefu za Kanisa hilo lililoko Oysterbay, Dar es Salaam.


"Wakati Katekista akinitaka nitoke nje, ghafla alinisukuma nikaanguka kwenye ngazi na kudakwa na mtu mwingine aliyeniokoa, la sivyo ningeumia vibaya," alidai.


Alidai kilichomsikitisha ni kudaiwa kutaka kuingia kanisani akiwa amevaa nguo zilizoacha mwili wazi, jambo ambalo si la kweli, kwa kuwa alikwenda kanisani hapo akiwa na kitambaa kilichofunika mwili.


"Nilipofika kanisani, nilikutana na Katekista akimrudisha mtu mwingine, ghafla alitokea bibi harusi aliyevalia nguo ambazo hazikuruhusiwa kanisani, akaniomba skafu niliyokuwa nayo, nikampa nami kubaki wazi mabegani," alidai.


Baada ya kuvua kitambaa hicho, alidai alitaka kuingia kanisani ili kuchukua funguo za gari, lakini alikutana na Katekista kwenye ngazi, ambaye alimwamuru atoke nje naye akaendelea kumsihi kuwa anakwenda kuchukua funguo za gari ndani, hata hivyo hawakukubaliana.


Aliendelea kudai, kuwa Katekista alipomsukuma na kuanguka, baada ya kudakwa alichanganyikiwa akidhani kanisani ni sehemu ya malumbano, akakimbilia ndani kutafakari, huku kiatu chake alichonunua nje ya nchi (Uingereza) kikiwa kimeharibika.


Alidai kuwa akiwa kanisani, Katekista alimfuata tena na kumsihi atoke nje, jambo lililosababisha ndugu zake wamzingire kiongozi huyo wa Kanisa na kumhoji kwa jazba, sababu ya kumsukuma ndugu yao na kuhatarisha maisha yake.


Baada ya malumbano huyo, alitoka nje ya Kanisa na kuacha utaratibu mwingine ukiendelea, huku akilalamika kwamba Kanisa ni sehemu takatifu hivyo hapatakiwi kuwa uwanja wa mapigano na kwamba limeacha kazi ya kufundisha na kuomba ielezwe wazi watu wavae nini.


Akijibu tuhuma hizo, Katekista Maboko alimpongeza mwandishi kwa kushuhudia tukio hilo na kutoa habari yake na kuongeza kuwa utaratibu wa jinsi ya kuingia kanisani kwa maharusi, umekuwa ukifundishwa tangu kuandikishwa kwa ndoa hadi mafundisho ya ndoa.


Alisema dada huyo alipofika kanisani hapo, alikuwa na wanawe wawili waliokuwa na mavazi yaliyoacha sehemu za miili yao wazi, na aliwaelewesha lakini yeye akabisha.


"Niliwashika mikono na kuwapeleka uliko ubao ili wasome maelekezo ya kinachotakiwa kuvaliwa, lakini yeye alilazimisha kuingia huku akisema Mungu haangalii mavazi, bali roho," alisema Katekista Maboko na kuongeza kuwa wakati akieleza hayo, ndipo wanandugu walipofika na kumhoji.


Kuhusu miwani yake kuvunjwa, alisema wakati akiwa amezungukwa na watu kama 30 kwa lengo la kumchanganya, aliendelea kujenga hoja kuwa kanisani zipo taratibu zinazotakiwa kuzingatiwa, lakini mmoja wao alitumia nguvu na kuvunja miwani hiyo.


Hata hivyo, alisema mtu huyo aliomba samahani na kulipa kiasi cha fedha, ambapo walipeana mikono kama ishara ya kusameheana.


Katekista Maboko alisema kwa ufupi kilichotokea, ni kukosekana kwa busara kwa waumini hao, kwani vipo vibao vinavyotoa maelekezo juu ya utaratibu unaotakiwa na unaopaswa kufuatwa


Wednesday, July 24, 2013

FFU wapinduka na mmoja afariki

ASKARI mmoja wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) Mkoani Kilimanjaro, Fidelis Mwaliyatabu, amefariki dunia papo hapo na wengine tisa akiwamo Mkuu wa Kikosi hicho kujeruhiwa vibaya baada ya gari lao kupinduka katika kijiji cha Kilingi, wilaya ya Siha, wakati wakienda kuzima vurugu za wananchi.

Ajali hiyo ilitokea wakati kikosi hicho kikielekea katika kijiji cha Karansi kwa ajili ya kukabiliana na wananchi waliokuwa wakiandamana kupinga wenzao waliokamatwa usiku wa manane baada ya kuvamia mashamba mali ya Shirika la Roho Mtakatifu-Kilasara.

Taarifa kutoka kijijini humo zilieleza kwamba wanakijiji waliamua kuandamana baada ya wenzao watano kukamatwa na Jeshi la Polisi nyakati za usiku kwa mahojiano kutokana na kukabiliwa na tuhuma za kushawishi wanakijiji wenzao kuvamia maeneo ya Shule ya Kilasara na kusababisha hasara kubwa kwa shule hiyo.

Kufuatia kukamatwa kwa watuhumiwa hao, wanakijiji waliamua kuaandamana hadi katika kituo cha polisi ili kuwatoa wenzao hali ilisababisha jeshi hilo kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya, jambo ambalo lilishindikana kutokana na wingi wa watu walikuwa wanaandamana.
Inadaiwa kuwa wananchi hao walijikusanya na walianza kuandamana kuanzia majira ya saa 7 usiku kuelekea kituo cha polisi ili kuwatoa wenzao walikuwa wanashikiliwa.

Wananchi wanaoshikiliwa na jeshi hilo ni John Sokoine, Abeli Solomoni, Christopher Solomon na aliyetambuliwa kwa jina moja tu la Julius. Wote walikamatwa usiku wa kuamkia jana.

Mnamo Juni 11, mwaka huu majira ya mchana wananchi wa kijiji hicho walivamia eneo lenye ukubwa wa hekta mbili na kufyeka mazao mbalimbali yaliyokuwa shambani hapo kwa madai kuwa wamiliki wa shule hiyo wamechukua eneo hilo kinyume cha taratibu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shirika la Roho Mtakatifu, Kanda ya Afrika, Padri Jerome Okama, aliushutumu uongozi wa kijiji hicho kwa kuvifumbia macho vitendo vya wananchi kujichukulia sheria mkononi wakati wakitambua kuwa eneo hilo lenye ukubwa wa hekta 8.9 linamilikiwa na shirika hilo kihalali.

Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Robert Boaz, alisema askari hao walipata ajali hiyo majira ya saa 6.45 mchana katika kijiji cha Kilingi nje kidogo ya mji wa Sanya Juu.

Alisema askari hao wamelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC na wengine wamelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Ugonjwa wa Kifua Kikuu ya Kibong'oto ilioyopo wilayani Siha na kwamba watano kati yao hali zao ni mbaya.

Alitaja gari la Polisi lililopinduka na kuua kuwa ni Toyota Land Cruiser lenye namba PT 2070 lililokuwa likiendeshwa na Sajenti Herman Dancan. Chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi na kuacha njia na kupinduka.

Aliwataja waliojeruhiwa katika ajali hiyo kuwa ni Mkuu wa FFU mkoani hapa, ASP Nonino, Renatus Misigalo, Alfonce Joseph, Koplo Elifuraha Lenare, Peter Albert, Bashiri Yusuph, George Mwakyusa na Gaspar Mwapunda.

Alisema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya Kibong'oto.

Sumaye awaonya watanzania

Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye amewatadharisha Watanzania kuwa makini na watu wanaotaka Madaraka kwa kugawa fedha katika sehemu mbalimbali za nchi au majimboni akionya kwamba wanaweza kujikuta wakimweka madarakani kiongozi anayejihusisha na biashara ya dawa za kulevya.

"Hivi kama mtu anaweza kuhonga sehemu kubwa ya wapigakura katika jimbo la uchaguzi au hata katika nchi kama nafasi anayosaka ni urais; tumeshajiuliza hizo fedha nyingi hivyo anapata wapi? Kama anajihusisha na biashara hizo chafu akipata nafasi hiyo watoto wetu watapona?"alisema Sumaye jana na kuongeza:

"Haya ni maswali muhimu ya kujiuliza tunapoelekea mwaka kesho kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa na mwaka 2015 wakati wa Uchaguzi Mkuu".Alisema hayo mjini Morogoro kwenye maadhimisho ya miaka 20 ya Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (Mviwata).

Akizungumza kwa tahadhari alisema haizungumzii Serikali yake iliyoko madarakani wala mtu yeyote, bali tabia mbaya, Sumaye alisema biashara ya dawa za kulevya inahusisha fedha nyingi na mitandao mipana ambayo isipodhibitiwa inaweza kulitumbukiza taifa katika janga.

Alisema Katiba Mpya siyo mwarobaini wa matatizo yanayolikabili taifa bali, utekelezaji na usimamizi wa sheria na kwamba jambo muhimu ni kuwa na Serikali itakayosimamia na kutekeleza sheria ili kulinda yale yaliyoelekezwa katika Katiba.

Katiba haiwezi kumzuia mwizi kwenda kuiba na sheria haitamzuia mwizi kwenda kuiba ila itatamka adhabu ya kupewa huyo mwizi.Kwa hiyo ili vyote hivi viwe na maana ni lazima awepo mtu au chombo cha kumkamata huyo mwizi na kumfikisha katika mikono ya sheria na chombo hicho ni Serikali.

Kama haiwezi kufanya hiyo kazi kwa ukamilifu tutaishia kulalamika tu na maonevu na maumivu yataendelea kuumiza jamii.Kwa hiyo hata Katiba iwe nzuri namna gani na ikatamka kuwa rushwa ni adui wa haki na hata ikatoa adhabu kali sana kwa kosa hilo; kama tutaweka viongozi madarakani kwa rushwa, hiyo Katiba wala haitatusaidia.

Hivyo Katiba nzuri mpya lazima iambatane na Serikali safi yenye kusimamia masilahi ya umma. Huwezi kumweka madarakani mwenyekiti wa kijiji au diwani au mbunge au hata Rais kwa rushwa ya kuwanunua wapigakura halafu utegemee Katiba Mpya itajibu matatizo ya jamii.

Azungumzia Mviwata Sumaye alisema Mtandao huo wa Wakulima Wadogo Tanzania ndiyo unaojua tatizo la kilimo na shida zao na ndiyo unaotakiwa kuulizwa cha kufanya ili kilimo chetu kibadilike na mkulima afaidike...

"Kama hatuwahusishi na kuwashirikisha katika sera, mipango na programu za kilimo, basi tujue kuwa sera, mipango na programu hizo zitashindwa".

Alisema Tanzania ni nchi ambayo wananchi wake wengi wanategemea kilimo kwa maisha yao na uchumi wa taifa pia kwa kiasi kikubwa hutegemea sekta hiyo, lakini bado ni duni na hakijamkomboa mkulima mwenyewe wala uchumi wa taifa...

"Nchi na watu wake bado ni maskini pamoja na kuwa watu wachapakazi wapo na ardhi kubwa na nzuri yenye rutuba ipo".

Alisema suala la usindikaji wa mazao lazima lipewe kipaumbele vinginevyo kilimo hakitamwondoa mkulima katika umaskini.Kama tutaendelea kuuza mazao ghafi ambayo bei yake katika masoko ya nje ni duni na haitabiriki, basi wakulima wetu na uchumi wa taifa letu vitazidi kudidimia. Mazao yaliyoongezwa thamani kwa usindikaji yanapata bei nzuri na usindikaji nao pia hutoa ajira kwa watu wetu.

"Kwa mfano, badala ya kuuza pamba ghafi tubadilishe pamba yetu kuwa nyuzi na vitambaa, katani yetu iwe katika kamba na mazulia, chai na kahawa ziwe katika paketi za kutumia, matunda yasindikwe katika makopo na kadhalika. Kwa msaada wa Serikali yetu, Mviwata inaweza kabisa kufanya kazi hii ama peke yake au kwa kushirikiana na wadau wengine wa uwekezaji ili kujenga viwanda vya usindikaji mazao. Tusiisubiri Serikali peke yake haitaweza na tutajichelewesha" Alimalizia

Tuesday, July 23, 2013

Maneck ajichora Tattoo yenye jina la Ngwair

Producer Maneck wa Am Records yupo kwenye harakati za kumalizia kuchorwa Tatto ya Rafiki Yake wa karibu Marehemu Albert Mangweha.

Maneck amesema sababu za kuchora tatto hii ni kama kumbukumbu ya milele ya rafiki yake Ngwear. Walifahamiana kwa muda mrefu, wamefanya kazi pamoja na ni tendo la msingi yeye kuchora hii tatto.

Mpaka sasa haijakamilika Ila Soon atamalizia, Maneck Ana Tatto 7 Kwenye mwili wake hii ni ya 8. Hii Anachora mkono wa Kushoto ndio upande wa kuchora mambo ya muziki.

Sunday, July 21, 2013

Shilole aapa kumchapa Sintah

Muigizaji wa kike wa filamu na muziki Bongo zuwena Mohamed ‘Shilole’ amemtangazia hali ya hatari msanii mwenzake wa filamu na mtangazaji wa televisheni Christina John ‘ Sintah’ kuwa popote atakapomkuta lazima amchape kwa kipigo ambacho hatasahau katika maisha yake...


Shilole  ametoa kauli hiyo kufuatia kuandikwa na mwanadada huyo katika mtandao wake akimbeza kwa kejeli. .

“Ni kweli sisi wanawake hatupendani na kuwa na wivu wa kijinga, mtu anakurupuka anakotoka bila hata kufanya utafiti na kunibeza eti sina uwezo wa kuimba na JLO (Jenifer Lopez) ....


"Kuna mtu aliyetegemea mimi kwenda kufanya show Marekeni! Sasa ninachomwambia ninamtafuta nikikutana naye nimtapa kipigo cha Mbwa mwizi,”aliongea kwa hasira Shilole.



Katika mtandao wake Sintah aliandika kwa kusema Shilole ni sawa na mtu anayeota ndoto za mchana, na kumkejeli kwa kusema kuwa aendelee kuota anaweza baadae kurudi katika hali yake...


 Sehemu ya maneno yanayomkera Shilole ni haya:

“Shilole bwana hii week katujia na kali kuliko eti ameongea na Benny Medina (Jlo’s Manager) ili aweze kufanya collabo na my sister, heee yes inawezekana maana hakuna lisilowezekana chini ya jua lakini swali ni?? wataimbaje?? yule dada yake na mie ni RnB na music wa Shilole bado sijaujua ni chakacha ama nini sasa naomba msaada kwenye tuta wadau wa music, hili linauwezekano??,”

“ Chakacha na RnB?? Kwa sababu Shilole nyimbo zake sawa na Snura wa majanga, kidogo Linah angeniambia ana collabo na my sisy ningeelewa sasa Shilole?? Ndoto za mchana ila si vibaya kuota maana ukishtuka unarudi ktk reality,”


Shilole anasema kuwa hajawahi kumuona mwanamke mwenye roho dhaifu kama Sintah, anajifanya anambabaikia Jlo wakati hata hajulikani....


“Mimi sikuwa nimeenda Marekani kwa ajili ya kuomba kumshirikisha J-lo kuimba naye,  lakini baada ya meneja wake kuja kuniona na kumpelekea video za muziki wangu  JLO alikubali kufanya kazi na mimi...


"Ilitakiwa nionane naye siku ya Jumapili lakini ndio siku niliyoondoka na ninarudi huko kwa ajili ya kazi hiyo, sijui nikifanya naye kazi atajificha wapi?,” anasema Shilole.


Shilole anasema Mungu ni mkubwa hata kama kuna mtu anayemchukia kwa mafanikio yake bado Mungu ana nafasi kubwa kuwazima watu wenye roho mbaya wivu kama Sintah ambaye anaonekana yupo tayari kwa ajili ya kuwaombea matatizo watu wanaojituma kwa ajili ya kuendesha maisha yao.


Miili ya wanajeshi 7 kukabidhiwa kwa ndugu zao LEO JUMATATU

Miili ya wanajeshi saba wa jeshi la Umoja wa Afrika raia wa Tanzania ambao waliuawa kufuatia shambulio huko Darfur nchini Sudani imepokelewa jijini Dar es salaam nchini Tanzania tayari kwa taratibu za mazishi.

Miili hiyo imepokelewa kwenye uwanja wa anga la jeshi la wananchi jijini Dar es Salaam na kupokelewa kwa simanzi na wanajeshi wa JWTZ pamoja na ndugu jamaa na marafiki waliofika kwa wingi  uwanjani hapo.


Wakiwa na nyuso za maombolezo baadhi ya wafiwa wametoa wito kwa jumuiya za kimataifa na umoja wa Afrika kuwa makini kwa kuhakikisha usalama wa vijana na walinda amani wanaotumwa kulinda amani katika mataifa mbalimbali.


Msemaji wa JWTZ Meja Joseph Masanja amesema kuwa baada ya miili hiyo kuwasili taratibu mbalimbali za jeshi hilo zitafanyika na kisha miili hiyo itakabidhiwa kwa ndugu zao kwa taratibu za maziko.


Hapo awali Mwendesha mashtaka mkuu wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita ICC Fatou Bensuda ametoa onyo kali kuhusu shambulizi la hivi karibuni lililowalenga waangalizi wa amani kutoka Umoja wa Mataifa na jeshi la umoja wa afrika huko Darfur Sudan UNAMID na kusema kuwa linaweza kuhesabika kama uhalifu wa kivita.


Katika taarifa yake akiwa Heague Fatou Bensuda amekumbusha pande zote zenye mgogoro kufahamu kuwa mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita ina mamlaka jimboni Darfur.


Mnamo tarehe 13 mwezi Julai wanajeshi saba wa kulinda amani raia wa Tanzania waliuawa na wengine kumi na saba kujeruhiwa baada ya shambulizi kutekelezwa na kundi ambalo halijafahamika huko Darfur nchini Sudani.




Thursday, July 18, 2013

Siku ya Mandela leo kuadhimishwa na Yatima, Dar es Salaam

Ubalozi wa Afrika Kusini nchini, umepanga kuadhimisha Siku ya Mandela Duniani hii, kwa kushiriki shughuli mbalimbali za jamii katika kituo cha watoto yatima cha Maria Theresa Dar es Salaam.

Mshauri wa Balozi wa Masuala ya Siasa, Terry Govender, amesema watatumia dakika 67 kufanya kazi mbalimbali ndani ya kituo hicho kwa kushirikiana na watoto wanaolelewa mahali hapo.

Kwa mujibu wa Govender, Ofisi ya Habari na Mawasiliano ya Umoja wa Mataifa ndio iliyopendekeza kituo hicho kwa mwaka huu.

Kwa maelezo ya mshauri huyo wa siasa, mwaka jana ubalozi huo uliadhimisha siku hiyo kwa kufanya shughuli mbalimbali za kijamii katika Shule ya Msingi Tandale ya Dar es Salaam.

"Lengo letu ni kuwashawishi watu wote duniani wawe na utaratibu wa kujihusisha na shughuli za kijamii japo kwa dakika 67, ambazo tunaamini wanaweza kuzitenga na kufanya la maana katika maeneo watakayochagua.

"Siku ya Mandela haimaanishi kutoa msaada, bali kuwajibika kwa jamii katika shughuli mbalimbali. Tutaendelea kuitekeleza ili kuwavuta watu watenge muda wao kuwajibika katika shughuli za jamii," alisema na kuongeza kuwa wataanza kazi kwenye kituo hicho saa 3:30 asubuhi.

Alitaja kazi watakazozifanya kuwa ni kupasua kuni katika magogo yaliyohifadhiwa, ili zitumike kupika kwa urahisi, kukata mboga na kuandaa chakula (kupika), kufanya usafi wa eneo hilo na shughuli nyingine za jamii zitakazo kuwepo wakati huo.

Siku ya Mandela Duniani ilitangazwa rasmi Novemba 2009 na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UN), ikilenga kushawishi  jamii duniani kutenga muda kwa kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii.

Kutangazwa huko kwa siku hiyo kulizingatia kujitoa kwa Rais mstaafu wa Afrika Kusini, Nelson Mandela katika shughuli za jamii, ambapo, kwa miaka 67 mfululizo amekuwa akizifanya bila kuchoka.

Rais Kikwete achonga na Rais wa Sudan kuhusu vifo vya askari 7

Rais Jakaya Kikwete amefanya mazungumzo kwa njia ya simu na Rais wa Sudan, Omar Bashir, kuhusu kuuawa na kujeruhiwa kwa askari wa Tanzania, walioko katika ulinzi wa kimataifa wa amani katika jimbo la Darfur.

Taarifa ya Ikulu iliyotumwa kwa vyombo vya habari jana, imeeleza kuwa katika mazungumzo hayo, Rais  Kikwete alimtaka Rais Bashir kuchukua hatua za haraka kuwasaka na kuwakamata waliohusika na kitendo hicho kiovu, na kuwafikisha mbele ya sheria haraka iwezekanavyo.

Rais Bashir amekubaliana na Rais Kikwete na kumuahidi kuwasaka hadi kuwakamata wale wote waliohusika na kuwachukulia hatua za kisheria.

Alimueleza Rais Kikwete kuwa binafsi anaamini waliohusika ni wahalifu, kusisitiza kuwa lazima watasakwa hadi kukamatwa na kuchukuliwa hatua.

Alimpa pole Rais Kikwete kwa tukio hilo la kusikitisha, ambapo wanajeshi wa Tanzania walienda nchini Sudan kulinda amani na usalama wa wananchi wa Sudan.

Awali Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Ki-moon, alimpigia Rais Kikwete na kumpa pole kwa mkasa huo mkubwa na wa kusikitisha, ambao umewatokea Watanzania hao wakati wakitekeleza jukumu lao la kulinda amani nchini Sudan.

Hadi sasa hakuna kikundi chochote kilichokiri kuhusika na shambulio hilo, ingawa kumekuwa na hali ya kutupiana lawama baina ya vikundi vya kiserikali na vya waasi katika jimbo la Darfur.

Mapigano baina ya vikundi vya kikabila na koo mbalimbali, yamesababisha mapigano na uvunjifu mkubwa wa amani na usalama katika jimbo la Darfur kwa muda wa miaka 10 sasa.

Mara nyingi mapigano na tofauti zao hizo zimesababisha vifo na uvunjifu wa amani kwa wananchi wa Sudan na wageni pia.


Mwishoni mwa mwaka jana wanajeshi wanne kutoka Nigeria, waliuawa karibu na El Geneina, Magharibi mwa Darfur, ambapo pia inaelezwa na AU kuwa wanajeshi wapatao 50, wameuawa tangu kikosi hicho cha Umoja wa Afrika kinachoundwa kwa chini ya Umoja wa Mataifa (UNAMID), kianze operesheni yake mwishoni mwa 2007.


Taarifa za UN pia zinaeleza kuwa kabla ya mashambulizi yaliyofanyika dhidi ya kikosi cha Tanzania Jumamosi iliyopita, wanajeshi sita wanaolinda amani waliuawa tangu Oktoba mwaka huu, ambapo pia inasadikiwa kuwa watu wapatao 300,000 wameyakimbia makazi yao.


Hata hivyo, kiini cha mgogoro huo inasadikiwa kuwa ni ugomvi wa ardhi na rasilimali zilizoko katika jimbo hilo nchini Sudan.


Miili ya maaskari hao saba wa Tanzania, inatarajiwa kuwasili nchini kwa ajili ya maziko.

Wanafunzi 22 wafariki baada ya kula chakula chenye sumu shuleni

Takribani watoto 22 wamekufa na wengine wengi wanaumwa baada ya kula chakula cha bure shuleni mchana ambacho kulichanganyika na dozi kubwa ya dawa za kuua wadudu, maofisa nchini India walisema jana.

Haikuweza kufahamika mara moja jinsi kemikali hizo zilivyoingia kwenye chakula hicho kwenye shule moja iliyoko mashariki mwa jimbo la Bihar, ingawa mmoja wa maofisa alisema inawezekana chakula hicho hakikuwa kimeoshwa vema kabla ya kupikwa.

Watoto hao, wenye umri wa kati ya miaka 8 na 11, walianza kuumwa juzi muda mfupi baada ya kula chakula cha mchana shuleni kwao huko Masrakh, kijiji kilichopo maili 50 kaskazini mwa mji mkuu wa jimbo hilo wa Patna.

Mamlaka za shule hiyo haraka zikasitisha kugawa chakula hicho cha wali, soya, dengu na viazi kufuatia watoto hao kuanza kutapika.

Chakula hicho cha mchana, sehemu ya kampeni maarufu ya nchi nzima kuwapatia chakula japo mlo mmoja watoto kutoka familia masikini, kilikuwa kimepikwa kwenye jiko la shule hiyo.

Watoto hao haraka walikimbizwa kwenye hospitali moja mjini humo na baadaye wakapelekwa Patna kwa matibabu, alisema msemaji wa serikali Abhijit Sinha.

Mbali na watoto hao 20 waliokufa, wengine 27 akiwamo mpishi wa shule walipelekwa hospitali, alisema. Kumi kati yao walikuwa katika hali mbaya.

Mamlaka zimemsimamisha kazi ofisa anayeshughulikia mpango wa mlo wa bure kwenye shule na kufungua kesi ya uzembe dhidi ya mwalimu mkuu wa shule hiyo, ambaye alitoroka mara baada ya wanafunzi hao kuanza kuumwa.

P.K. Sahi, waziri wa elimu wa jimbo hilo, alisema uchunguzi wa awali umeonesha chakula hicho kilikuwa na kemikali ya organophosphate inayotumika kuulia wadudu kwenye mazao ya mpunga na ngano.

Inaaminika nafaka hiyo haikuwa imeoshwa kabla ya kupelekwa shuleni hapo, alisema.
Hatahivyo, wanakijiji walisema tatizo linaonekana kuwa upande wa chakula cha soya na viazi, wakaongeza kwamba watoto ambao hawakula chakula hicho walisalimika - ingawa walikula wali na dengu.

Mpango wa chakula cha mchana nchini India ni moja ya mipango mikubwa duniani ya lishe mashuleni.

Serikali za majimbo zina uhuru wa kuamua aina ya chakula na mida ya mlo huo kutegemea hali ya eneo husika na upatikanaji wa chakula hicho.

Kwa mara ya kwanza ilianzishwa kusini mwa India, ambako kulionekana kuwapo wazazi wengi mafukara wasio na uwezo wa kuwapeleka watoto wao shule.

Tangu hapo mpango huo umekuwa ukisambaa nchi nzima na kuwasikia zaidi wa watoto wa shule milioni 120 kama sehemu ya juhudi za kukabiliana na utapiamlo.

Kwa mujibu wa serikali hiyo, karibu nusu ya watoto nchini India wanasumbuliwa na utapiamlo.

Ofisa wa ngazi ya juu aliyechaguliwa wa Bihar, Waziri Mkuu Nitish Kumar, ameamuru uchunguzi ufanyike kuhusu vifo hivyo.

Wednesday, July 17, 2013

'Foolish age' ya Lulu

Baada ya kujinyakulia tuzo ya msanii bora wa kike kutoka Zanzibar International Film Festival 2013 (ZIFF) kupitia filamu ya woman of principle, Elizabeth Michael aka Lulu anatarajia kuja na filamu yake mpya itakayoitwa “foolish age”.
Kupitia filamu ya woman of principle, Lulu alijiongezea umaarufu na kuonyesha uwezo mkubwa wa kushirikiana na mastaa wa kubwa kama Ray na Nargis. Foolish age itajaa mastaa mbalimbali wenye uwezo mkubwa wa bongo movie.
Lulu bado ajafunguka sana kuhusiana na location ya foolish age wala tarehe itakayo dondoka sokoni.

Tuesday, July 16, 2013

Prezzo:SIWEZI MUOMBA DIAMOND MSAMAHA

Habari kutoka Kenya ni kwamba msanii Prezzo amesema hatoweza kumuomba msamaha msanii kutoka Tanzania Diamond Platinumz  kwa kuwa yeye Diamond ndiye aliyeanza kumkashifu Prezzo.

Leo mchana Prezzo akiongea na ‘Mzazi’ Willy M. Tuva’s award-winning show, alisema “Mimi sipendi kuwa na adui kwa sababu muziki unafaa kuleta muungano, sa me
nikashangaa mbona huyu brother ananiingilia na huku sikumbuki kumkosea wala hatujawahi kukutana ana kwa ana”.
Prezzo aliendelea kusema “Mtu yeyote anamjua Prezzo ni kama rattle snake, ukimchokoza you have to get prepared to be bitten.


nilijaribu kumpigia simu lakini jamaa hakupokea simu nikaona ah! Basi liwalo na liwe, nikadecide ku-air my views”, revealed Prezzo.
Aliendelea kusema “Mimi siwezi kumuomba msamaha Diamond kwenye twitter na wala sitoweza kufanya hivyo kwa sababu ni utoto”.

Wanajeshi 7 waliofariki Sudan, wako njiani wanarejeshwa Tanzania

Wanajeshi waliofariki jumamosi iliyopita tayari miili yao imeagwa huko Darfur Sudan na wanasafirishwa kuja Tanzania kwaajili ya mazishi. Hizi ni baadhi ya picha zikiwaonesha wakati wakiagwa na kuweka katika gari kwaajili ya kusafirishwa na pia majeruhi waliolazwa.















Monday, July 15, 2013

CHADEMA kufungiwa usajili isipoifuta 'Red brigade' .

Ofisi ya msajili wa vyama vya siasa chini ya mwenyekiti wake Bwana John Tendwa imesema imesikitishwa na Chama cha CHADEMA kuanzisha kambi za mafunzo ya ulinzi (Red Brigade).


Ofisi hiyo ya msajili imekitaka chama cha CHADEMA kuachana na mpango wa mafunzo ya vikundi mara moja vinginevyo ofisi hiyo itakichukulia hatua kali, na hatua hiyo ni kukifutia usajili.


Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari imewataka wale wote wanaosema kuwa CCM inavyo vikundi vya ulinzi, wapeleke ushahidi huo na wao kama wasajili wa vyama vya siasa watakifungia bila kusita.


R.I.P mashujaa wa Tanzania

Majina ya askari saba wa Tanzania waliokufa  kwenye shambulio la ghafla mjini Darfur yamepatikana.


Askari hao waliokufa ambao walikuwa kwenye vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Mataifa huko nchini Sudan ni Sajenti Shaibu Othuman, Koplo Oswald Chaula, Koplo Mohamed Juma, Koplo Mohamed Chikilizo, Pte. Rodney Ndunguru, Pte. Peter Werema na Pte. Fortunatus Msofe.




Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana kwenye mtandao ni kwamba askari hao walikwenda kujaribu kumwokoa mwenzao (ambaye hakutajwa) ambaye alisemekana kutekwa na vikosi vya waasi nchini humo.



Wakati  wakijiandaa, ghafla walizingirwa na askari hao waasi na kisha kushambuliwa kwa risasi hadi kufa.
 


Haikufahamika hali ya askari huyo ambaye alidaiwa kutekwa kama bado yu hai ama ni miongoni mwa waliokufa.



Mungu azilaze roho za askari wetu mahali pema peponi, Amina.

Friday, July 12, 2013

PAULINE ZONGO, JOAN NA KIMOBITEL WAIBUKA NA NDEGE WA3


Hatimaye wanamuziki wakali nchini Tanzania waliotamba sana hapo nyuma kidogo wameunda kundi lao jipya linalojulikana kwa jina Ndege wa3, kundi jipya  linaloundwa na wanamuziki Joan matovolwa, Khadija Mnoga (Kimobitel) na Paulyne Zongo.

 Wanamuziki wakali haoa hivi karibuni wameshatoa kibao chao kinachokwenda kwa jina la 'MISUKOSUKO YA MAPENZI' ambacho redio kadhaa nchini zimeanza kukirusha.

MISUKOSUKO YA MAPENZI wamesema ni nyimbo ambayo imetungwa kwa umahiri wa hali ya juu, na kuonyesha viwango vya juu katika uimbaji na utunzi, na maudhui ya wimbo huu ni kuonyesha jinsi mapenzi yalivyo na majaribu katika maisha ya kila siku na jinsi ya kuikabili.

Kwa sasa Joan Matovolwa na Paulyne Zongo ni wanamuziki huru wakati Khadija Mnoga (Kimobitel) ni mwanamuziki anayeimba katika bendi ya Extra Bongo inayoongozwa na Camarade Ally Choki.

Mbali na wimbo huo, ndege 3 wamesema kuwa wamejipanga sana kwa nyimbo kali kutoka kwao , maana wamesema sauti za kuimba wanazo , uwezo wa kuimba wanao na sababu ya kuimba pia wanayo

Thursday, July 11, 2013

Pole Joyce Kiria kwa msiba wa baba yako!!


Kuhusu baba mzazi wa Joyce Kiria, Michael Francis Lwambo Kiria wa kibosho dakau nganyeni kufariki huko mkoani Tanga ambako alikuwa akiishi, naomba nitoe maneno kidogo ya faraja kwake.

Joyce Kiria Leo ni siku ambayo hutakaa kuisahau maishani mwako, kwa sababu majuzi tu ndo umetoka Tabora kumwona rafikiyo wa karibu sana, mumeo. Leo tena msiba wa baba yako, Pole sana dada yangu.

Kuna mambo nataka yakufariji;  Mungu anaweza kuonekana zaidi wakati wa furaha na amani na wakati wa shida asionekane kabisa.

Hapa nina maana kwamba Mungu yupo pamoja nasi kila wakati ila tunapokuwa na furaha na amani yeye huwa pembeni yetu na ndiyo maana unamuona, lakini tunapokuwa na woga au kupita katika shida na majaribu yeye hutuchukua na kutufunika na uwepo wake na ndiyo maana hatumuoni.So, hupaswi kuogopa chochote kwani yeye atakuvusha kwenye bonde la uvuli (Zaburi 23:1-6).
Joyce, kila jambo linalotokea hapa duniani liwe zuri au baya, iwe furaha au huzuni fahamu kuwa Mungu karuhusu. Mungu ndiye ajuaye sababu. Umesikia habari ya Ayubu, ndo maana tumeagizwa kushukuru kwa kila jambo.
 Mwisho, usimtafute mtu yeyote juu wakati huu ila MUNGU pekee. MUNGU NA AKUSAIDIE.

Mwenyezimungu aiweke roho ya marehemu mzee Michael Lwambo mahali pema peponi, Amina